PAMBAZUKO LIMEFIKA(SHAIRI)

https://novakambota.files.wordpress.com/2015/01/a964a-p3.jpg
Na Nova Kambota,
Sikulitunga shairi, mwaka mpya nikingoja
‘Shirini kumi na tano, siwezi tena kungoja
Katika taifa duni, chama cha vingi viroja
Huu ni mwaka kisasi, lazima tuwape somo
Tuukatae utumwa, tuuhini ukasuku
Siasa za fumwafumwa, akili za zumbukuku
Haki zetu tunanyimwa, mchana siyo usiku
Wanyonge tukiamua, watawala watajuta
Wapeni hizi salamu, wale walamba michuzi
Watalia kama mamba, ni mwaka wa mageuzi
Wanyonge tumeamua, kuondoa upuuzi
Siasa za kilaghai, mwisho wake umefika
‘Tapiga kura kisasi, uamuzi wenye tija
Oktoba ikifika, uzalendo utakuja
Unyonge tutaondoa, siasa za rejareja
Chama kinaumwa kansa, ni kansa ya uongozi

Giza tutaliondoa, magamba ‘tawakomesha
Nchi itapata dawa, vichwa watainamisha
Makada ‘tawapa somo, mfano wa washawasha
Pambazuko limefika, na wewe upambazuke.

Andrew Nyerere; Mwalimu angekuwepo angepinga ufisadi!

Nyerere

Andrew Julius Kambarage Nyerere
Kuna maswala kadha wa kadha yanayoikabili Tanzania kwa hivi sasa, miongoni mwa mambo haya ni sakata la akaunti ya Tegeta/Escrow, mchakato wa katiba mpya na mengine mengi. Mwandishi Nova Kambota amefanya mahojiano na Andrew Julius Nyerere ambaye ni mtoto wa kwanza wa baba wa taifa hayati Mwalimu Nyerere, fuatana naye katika mahojiano haya………………
1. SWALI; Kuna mambo kadhaa yaliyojitokeza siku za karibuni ambayo watu wanataka kufahamu manufaa yake kwa taifa, moja ya matukio hayo ni ziara ya Jafar Mermo Idd Amin mtoto wa rais wa zamani wa Uganda marehemu Idd Amin mwaka 2008, je ziara hiyo ambayo ilimkutanisha na Madaraka Nyerere walipozuru Butiama ilikuwa na manufaa gani kwa taifa?

JIBU; Kwa familia ya Mwalimu Nyerere na familia ya marehemu Idd Amin nadhani ilikuwa jambo zuri kuleta upatanishi, kuhusu kama taifa lilipata faida sijui. Aliongea Jafari kuhusu kuanzisha mfuko wa hela kuwasaidia wanajeshi walioathirika na vita vya Kagera(wa Uganda na Tanzania), pia nchi hizi mbili zilihitaji kupatanishwa , Jenerali Musuguri alikuwa anaongea katika redio miezi michache iliyopita, kwamba wanajeshi wetu walikuwa na hasira sana, kabla ya kufika Kyaka walikuwa wameshawaua watu 10,000(elfu kumi), Jenerali Musuguri yupo hapa Butiama, natamani kwenda kumuuliza kama hao wote waliouwawa walikuwa ni maadui kwasababu hii ilikuwa ni vita yetu ya kwanza, inawezekana makosa yalifanyika.

 

2. SWALI; Una maoni gani kuhusiana na mwenendo wa CCM iliyoasisiwa na Mwalimu Nyerere ambayo sasa baadhi ya viongozi wake wanatuhumiwa vikali kujihusisha na ufisadi? Hudhani ni sababu tosha kwa watanzania kuikataa CCM ikiwa inakiuka misingi ya kuundwa kwake?

JIBU; CCM iliamua kujiita Chama Cha Mapinduzi kwa maana ya mapinduzi yaliyofanyika Urusi au Uchina, kwa maana kwamba watu walio wengi wakiwa na njaa wataleta fujo za kuiangusha serikali kama wamechochewa au hata kama hawajachochewa. Iwapo CCM itaendeleza hayo mapinduzi wananchi wataendelea kuichagua, inategemea tu watu wangapi bado wanaamini inaendeleza mapinduzi, maoni yangu mimi siyo muhimu, watu waamue, na nadhani wanaweza kugawanyika katika maamuzi.

 

3.SWALI; Miaka ya karibuni kumekuwa na watu wanaohoji namna baba wa taifa Julius Nyerere alivyoaga dunia, baadhi ya wanasiasa wametilia shaka mara kadhaa kifo chake mpaka ikampelekea Madaraka Nyerere kutoa kauli, vipi mtazamo wako kuhusu hili? Kuhoji kifo cha Nyerere kuna maslahi yoyote kwa taifa?

JIBU; Magige , mtoto wa Mwalimu anasema kuna chanjo moja ilikuwa wapewe watanzania ambayo Mwalimu alikuwa ana mashaka nayo. Mwalimu alimwambia Dr Mwakyusa kwamba yeye apewe, aijaribu halafu akiridhika ataiidhinisha wapewe Watanzania, lakini alipopewa hiyo chanjo, Mwalimu hali yake ilibadilika ghafla, amefariki. Niliposikia hiyo stori nilimweleza Magige kuhusu Global 2000 Report ya Warren Christopher, inasemekana katika miaka ya sabini viongozi wa Afrika walishauriwa na IMF wakubali wananchi wao wachanjwe chanjo za magonjwa ili watu wapungue ili iwe rahisi kuwasaidia; kwamba tatizo la kuwasaidia ni tatizo la logistics tu. Inasemekana ushauri huo ulikubaliwa na viongozi wetu. Global 2000 Report ni Top Secret ipo United Nations na hata ukiwa kule huwezi kuipata mpaka uwe na Special Clearence. No, nilimwambia Magige hatutapata faida yoyote tukianza kuuliza maswali kuhusu kifo cha Mwalimu, kama kuna mtu anabisha kwamba World Health Organization inaweza kufanya ufisadi, mtu huyo huwa anashauriwa kufanya utafiti jinsi W.H.O ilivyoanzishwa.

 

4.SWALI; Unazungumziaje mchakato wa kupatikana kwa katiba mpya nchini, kutokana na matukio yanayoendelea kujitokeza kama Mzee Warioba kupigwa na hali ya kutoelewana miongoni mwa watanzania, Je unaona wapi tumekosea? Nini kifanyike kunusuru mchakato huu ili tupate katiba itakayolivusha taifa letu kutoka hapa tulipo?

JIBU; Hakuna matatizo kuhusu katiba , isipokuwa kama kuna maoni yanayoweza kuiboresha katiba , maoni mapya ambayo siyo ya UKAWA , sasa ndiyo wakati wa kuyatoa.

 

5. SWALI; Unazungumziaje uongozi wa baba wa taifa hayati Mwalimu Nyerere? Una lipi la kusema kwa kumlinganisha na viongozi wa zama hizi?

JIBU; Sioni sababu ya kuwalinganisha viongozi wa awamu tofauti, zama tofauti zinahitaji viongozi, kumlinganisha Nyerere na Kikwete hiyo itakuwa sawa kumlinganisha Bismark na Angela Markel.

 

6.SWALI; Unazungumziaje harakati za vyama vya upinzani nchini kupambana na ufisadi kama wa hivi karibuni wa Tegeta/Escrow? Unadhani vyama hivi vya upinzani vina dhamira ya dhati kupambana na madudu?Je vitafanikiwa?

JIBU; Vyama vya upinzani vina nia njema , hii kashfa inayojadiliwa sasa hivi Bungeni imeletwa na upinzani. Hii vita ya sasa hivi ya Bungeni wanaweza kushinda, lakini kushinda uchaguzi wa serikali za mitaa ni jambo lingine.

 

7.SWALI; Kadri ulivyomwelewa hayati Nyerere, unazungumziaje kutokuwepo kwake? Je unadhani angekuwepo angesaidia vipi kunusuru taifa kwenye kupambana na ufisadi na kunusuru mchakato wa katiba mpya?
JIBU; Mwalimu angekuwepo angepinga ufisadi, kuhusu katiba hakuna tatizo kubwa au naweza kusema hakuna tatizo lolote zaidi ya fujo inayoletwa na UKAWA.

 

8.SWALI; Ukipewa nafasi ya kuwashauri vijana wa sasa wa Tanzania, ungependa wafanye nini kulisaidia taifa lao?

JIBU; Vijana wa Tanzania wafikiri sana kabla ya kuwachagua viongozi.

 

9.SWALI; Unapata tafsiri gani unapoona taasisi za kidini kama kanisa katoliki likianzisha, kusimamia na kuratibu mchakato wa kumtangaza hayati Mwalimu Nyerere kuwa Mtakatifu?

JIBU; Kanisa katoliki ndiyo linataka Mwalimu aitwe lay saint, Mwalimu aliishi maisha ya uadilifu lakini kama alikuwa mtakatifu hiyo ni kwa Vatican kuamua.

 

10.SWALI; Unaweza kueleza nini kuhusu siku za mwisho za uhai wa Mwalimu na namna alivyokuwa akilalamikia ubinafsishaji/uuzwaji wa mashirika ya umma kama benki ya taifa ya biashara NBC, ukizingatia hali ya ugonjwa wake na uzalendo wake kwa nchi, alikuwa mtu wa namna gani? Alionekanaje nyakati zile?

JIBU; Uuzaji wa mashirika ya umma au ubinafsishaji siyo jambo baya wakati wote.
Swali; una lolote la kumalizia?
Jibu; Kwa kumalizia, nataka kusema viongozi wachaguliwe kwa uadilifu, kwasababu ukiwachagua mafisadi, Mungu ataheshimu uteuzi wako, hatabadili kitu chochote!

 

Andrew Nyerere anaweza kupatikana kwa namba 0718- 536281, ikiwa unataka kuwasiliana na Nova Kambota mwandishi aliyefanya mahojiano haya piga simu namba 0712-544237, barua pepe; novakambota@gmail.com au tembelea https://novakambota.wordpress.com

Go Pinda,nenda tu mzee wangu,mpe fursa JK aunde baraza jipya!


Na Nova Kambota, 0712- 544237

Tofauti na wengi wanavyodhani, mzee wangu Pinda ulishaonyesha dalili za wazi ikiwa kweli unamudu vyema nafasi ya uwaziri mkuu. Kuna mengi tu yaliyofanya baadhi yetu tutilie shaka umahiri wako lakini hii skandali ya Tegeta/Escrow imefunga mjadala!
Unakumbuka uliposema na wapigwe tu? Liwalo na liwe!
Wakumbuka ile kauli ya tumechoka?
Wakumbuka mgomo wa madaktari?
Je wakumbuka kauli yenye utata “anayeua albino na yeye auwawe”?
Lakini wajua namna “mchwa” katika baadhi ya halmashauri wanavyotafuna fedha za wananchi?
Tegeta/Escrowni hitimisho la yote haya, mzee wangu Pinda mtoto wa kulima, let it go! Jiuzulu, mpe fursa rais Kikwete aunde baraza jipya la mawaziri, urais unaweza kutafutwa hata nje ya uwaziri mkuu!
Ukiwa mwanasheria utanielewa vizuri naposema hoja si ikiwa unahusika au la! Hili si muhimu sana, hoja hapa ni dhamana ya uongozi kusimamia shughuli za serikali ilishindwa kutumika kunusuru “skandali”hii. Kiongozi waumma “kutuhumiwa” si jambo jema, tuhuma pekee zinatosha kukufanya ubwage manyanga “resigning does not mean you are weak, but sometimes it means you are strong enough to let it go”
Achia ofisi ya umma kwa manufaa ya walala hoi wa Tanzania, kiongozi wa umma umetuhumiwa kutosimama kidete kuzuia uozo huu kabla, kauli za “kila mtu atabeba msalaba wake” si za kulisaidia taifa, ni kauli inayoashiria hamu ya mtawala asiyependa kuwajibika, anayetaka kung’ang’ania madaraka! Haifai kabisa, busara inakutaka kuwajibika kama mtangulizi wako Edward Ngoyai Lowassa, kumbuka “Caesar’s wife must be above suspicion’’
novakambota@gmail.com , https://novakambota.wordpress.com

WANYONGE MKIUNGANA-SHAIRI

https://novakambota.files.wordpress.com/2014/11/38e42-mtotoooooo.jpg
Na Nova Kambota, +255712 544237
Jumapili, 16 Novemba 2014
Dar es salaam, Tanzania.
Tano miongo yapita, taifa ladidimia
Wengi wameshastuka,dawa wajitafutia
Viongozi kadhalika, mali walimbikizia
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Tazama kwenye ramani, utaona hiyo nchi
Nchi ya wasio soni, wenye tabu wananchi
Raia wapo kinuni, watwangaji wana mchi
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Chama kisicho na dira, kimekamata hatamu
Wanakula kwa papara, hamu ya kula utamu
Roho zao za harara, mikono yao ya damu
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Wameileta rasimu, bila maoni ya watu
Kutawala wana hamu, roho zimekosa utu
Chama kisicho nidhamu, mfumo wake wa kutu
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Unganeni masikini, mijini na vijijini
Zinduka jitambueni, enyi tabaka la chini
Mmefanywa kuwa duni, jitoeni kitanzini
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Ondoeni hilo giza, enyi wana afrika
Hakuna cha kubakiza, pigeni kura ya zika
Nchi yazidi kuviza, inakumbwa na gharika
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Si dawa si pembejeo, hazipo tele nchini
Heri jana sio leo, taifa la watu duni
Amebanwa kwa koleo, hana hali masikini
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Zindukeni kina mama, mlete mabadiliko
Kataeni hiko chama, cha hao wavuta kiko
Idondosheni zahama, kataeni matambiko
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Vijana msitumike, bendera fata upepo
Lazima mmakinike, msiwe mfano popo
Pigeni ngumi na teke, hao walamba makopo
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata

Tamati nimefikia, beti kumi natulia
Wavuja jasho sikia, mwongozo fatilia
Unyonyaji kukataa, nchi ipate kupaa
Wanyonge mkiungana, minyororo mtakata.

Mtunzi wa shairi hilini Nova Kambota, ni mchambuzi na mwandishi wa siasa anayeishi jijini Dar es salaam, anapatikana kwa simu 0712-544237 , barua pepe; novakambota@gmail.com , waweza kutembelea Blog yake; https://novakambota.wordpress.com

Mapinduzi ya umma Yataendelea Kushamiri barani Afrika

http://t0.gstatic.com/images?q=tbn:ANd9GcRIS7V_0IddRq2tJGGaogUQXZJvQKwl_ksvqtQPuA6kDaXPEEbVSQ
Kuelekea 2030 serikali nyingi za kusini mwa jangwa la Sahara zitang’olewa
Na Nova Kambota, 0712 544237
Alhamisi, 13 Novemba,2014
Dar es salaam, Tanzania
Habari kubwa hivi sasa barani Afrika ni mapinduzi ya umma yaliyofanyika Burkinafaso, makala haya ni mtazamo wangu kuhusu kitakachojiri kusini mwa jangwa la sahara kuelekea 2030, mtazamo huu umejikita katika kutathimini matukio yanayoendelea kusini mwa jangwa la sahara na hali ya kisiasa kwa ujumla, fuatana nami katika maandishi haya ya kusisimua;
Kusini mwa jangwa la Afrika si salama
Dalili za wazi zinaonyesha kuwa nchi nyingi za kusini mwa jangwa la Sahara zipo katika hali mbaya zaidi ya nchi za kiarabu zilizopinduliwa kama Misri na Tunisia , halikadhalika kwenye mataifa hayo ya kusini mwa jangwa la sahara kuna ukosefu mkubwa zaidi wa ajira hivyo kufanya idadi kubwa ya vijana kuwa wazururaji kuliko Burkinafaso ambayo imepinduliwa hivi karibuni. Sasa ikiwa hali iko hivi kwanini viongozi wa mataifa ya kusini mwa jangwa la Sahara hawachukui tahadhari? Kwanini wanazidi kujisahau?
Viongozi wengi wa kusini mwa jangwa la sahara wanategemea kuudhibiti upinzani kwa msaada wa vyombo vya dola mfano mzuri ni hujuma kubwa dhidi ya viongozi wa upinzani kwenye baadhi ya mataifa yanayounda jumuiya ya Afrika Mashariki. Tatizo kubwa la marais hawa nikule kudhani kuwa vyombo vya dola vinaweza kuudhibiti umma, wanapaswa kujifunza kwa makini maana halisi ya nguvu za umma na athari zake kwa muktadha wa siasa za taifa lolote ulimwenguni, yatosha kuzingatia kuwa umma haujawahi kushindwa.
Vyama vingi tawala vitakataliwa
Kutokana na kushindwa kutimiza wajibu wake kwa wananchi vyama vingi tawala vitakataliwakatika mataifa ya kusini mwa jangwa la Sahara. Kuanzia miaka ya 1990 vuguvugu la vyama vya upinzani limeweza kuving’oa vyama tawala kadha wa kadha mifano ya UNIP Zambia, KANU Kenya na PDS Senegal hapa pia usisahau kuangushwa kwa chama cha UMD cha Fredrick Chiluba huko Zambia kilipopoteza kwa Michael Satta wa PF.
Angukohili la vyama tawala halikwepeki hasa kwa kuzingatia udhaifu wa vyama hivyo katika kushughulikia shida za wanyonge ikiwamo bei za mazao, ajira na kupanda kwa gharama za maisha, utegemezi mkubwa wa nchi za kiafrika kwa wawekezaji kutoka nje ,uwekezaji ambao umeshindwa kuondoa umasikini una kila dalili mbaya kwa vyama vya ANC Afrika Kusini, FRELIMO Msumbiji na CCM Tanzania, kuelekea 2030 vyma hivi vimezidi kupunguza idadi ya kura huku upinzani ukizidi kushika kasi kwenye nchi zao.
Marais ving’ang’anizi watang’olewa kabla ya 2030
Mwanahistoria Jovitus Mwijage katika kitabu chake “Major Events in African History” akielezea kushindwa kwa viongozi wengi waliotwaa madaraka kwa njia za mapinduzi mwishoni mwa miaka ya 1980 na mwanzano mwa miaka ya 1990 , katika ukurasa wa 308 anasema “Under the auspices of the constitutions made by them (African dictators), the ballots could not change the existing leadership; therefore, the barrel of the gun eventually became answer to those political puzzles. Even the constitutions made after the coups could not attend to the interests of the masses.The leaders of the coups made the constitutions, which were to ensure that their evil interests were fulfilled. Such constitutions appeared in Uganda, Sudan, Angola, Congo, Zimbabwe, Gabon, Togo and Rwanda”.
Hali hii ya viongozi kadhaa wa kiafrika ambao awali walionekana kuwa wawakilishi wa kweli wa wananchi lakini polepole wakazivunja miguu katika za nchi zao ili waendelee kutawala hivyo kugeuka ving’ang’anizini sababu nyingine itakayopelekea mapinduzi kwa nchi hizo. Iwe ni mapinduzi ya umma ama vinginevyo lakini marais ng’ang’anizi kama Yoweri Museveni wa Uganda na mwenzake Paul Kagame wa Rwanda wamekalia kuti kavu kwani wananchi hawataki ufalme ama usultani bali wanataka demokrasia inayozingatia ukomo wa madaraka. Ikiwa watawala wa mataifa haya wataendelea kukaa madarakani basi joto kisiasa halitawaacha salama, wimbi la mabadiliko litawafagia mmoja baada ya mwingine kuelekea 2030.

 

Nova Kambota ni mchambuzi na mwandishi wa siasa, hii ni sehemu ya maoni yake ya hivi karibuni kuhusu mapinduzi ya umma na mwelekeo wa siasa katika mataifa ya kusini mwa jangwa la Sahara. Nova Kambota anapatikana jijini Dar es salaam, simu +255712 544237, barua pepe; novakambota@gmail.com , Blog; https://novakambota.wordpress.com

Katiba ya Wananchi – (Shairi)


Na Nova Kambota,
0712 -544237, Alhamisi, Novemba 6, 2014

Katiba ya wananchi, mwafaka wa taifa
Kuna kucha hakukuchi, isije kuwa maafa
Kuandika ya kukidhi,yahitaji maarifa
Katiba ya wananchi, nauliza tutapata?

Iokoe wakulima, wavuvi na walemavu
Uchumi ukue hima, iondoe udumavu
Ilinde raia wema, viongozi wasikivu
Katiba ya wananchi , nauliza tutapata?

Watawala watambue, kilio wakisikie
Ukasuku waambae, waikatae ya kale
Machakato uenee, na demokrasi ikue
Katiba ya wananchi, nauliza tutapata?

Kukaa peke Dodoma,kuichambua rasimu
Kilio cha kina mama, haki zao ni adimu
Ile siku ya kiama, waso haki ni dhalimu
Katiba ya wananchi, nauliza tutapata?

Beti tano nakomea, kalamu naweka chini
Katiba kuongelea,sitachoka ulimini
Tunataka ya kumea, iuondoe uduni
Katiba ya wananchi,nauliza tutapata?

Barua kwako Mzee Joseph Sinde Warioba!

https://i0.wp.com/www.mwananchi.co.tz/image/view/-/2294864/highRes/735002/-/maxw/600/-/9lvs31z/-/warioba+px.jpg
Na Nova Kambota, Jumatatu Novemba 3, 2014
Shikamoo mzee wangu Warioba na pole sana kwa masaibu yaliyokukuta jana .
Mimi mjukuu wako pasi na shaka ukiangalia kwenye diary yako utanikumbuka kwani niliwahi “kukutupia” swali moja pale chuo kikuu Mzumbe siku ya tarehe 16 mwezi Novemba 2011.
Tangu hapo hatujapata kuonana tena ingawaje nimekuwa nikifatilia harakati zako zote tangu hapo? Kwanini nimekuwa nikifatilia? Jibu ni moja tu, kwa namna ulivyonijibu siku ile sikutia shaka uelewa wako mkubwa sambamba na uzalendo wako usio na doa kwa taifa hili.
Ulizidi kunifurahisha zaidi kwa namna ulivyoratibu mchakato wa kukusanya maoni ya katiba mpya na uandaaji wa rasimu. Najua wapo baadhi ya “wakubwa” hawafurahishwi na namna unavyotetea kile unachoamini ni chema kwa vizazi vijavyo vya Tanzania, Mungu akubariki sana.
Vitimbi ulivyofanyiwa na maneno ya kejeli uliyojibiwa yanaonyesha kuwa hayajakuvunja moyo hata kidogo, kwani jana nilikuona ukiongea kwa uso uliojaa bashasha huku ukidhihirisha kuwa ungali na ari ileile ya kupigania katiba ya wananchi.
Sitaki kukuchosha kwa maneno mengi mzee wangu lakini nina uhakika Mungu yuko upande wako katika hili, tuliotega sikio na kukusikiliza tunajua unaongea ukweli mtupu na MSEMA KWELI NI MPENZI WA MUNGU.
Hata manabii walipingwa na kudhihakiwa hivyohivyo lakini leo tunawasoma na kuwaheshimu kama mashujaa wa imani, ni ukweli kuwa katiba lazima iwe mwafaka wa kitaifa na siyo mpasuko wa kitaifa, wanaokupinga wanalijua hili?
Wasalam,
Ni mimi Mjukuu wako mtiifu,
Nova Kambota
0712-544237, novakambota@gmail.com , https://novakambota.wordpress.com

Rais Guy Scott wa Zambia; jaribio lingine kwa wahafidhina wa Afrika!

https://i0.wp.com/nehandaradio.com/wp-content/uploads/2013/05/Mugabe-and-Guy-Scott-e1367541327389.jpg

Rais Guy Scott wa Zambia akiwa na Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe
Na Nova Kambota,
Ijumaa, oktoba 31, 2014
Dar es salaam-Tanzania +255712 544237

Alipochaguliwa Barack Obama kuwa rais wa taifa kubwa zaidi duniani Marekani, waafrika walifurahishwa na hali hiyo huku wakichagiza kuwa hiyo ilikuwa ni silaha dhidi ya ubaguzi kwa waafrika.
Obama ambaye ana asili ya Kenya alipongezwa hata na wahafidhina wa Afrika kwa kueleza kuwa hakuna watu wa asili wa Marekani isipokuwa jamii ya wahindi wekundu pekee, hivyo kulikuwa na kila uhalali wa mwanasiasa mwenye asili ya Afrika kuliongoza taifa hilo.
Sasa ni kama vile kibao kimegeuka, sasa ni jaribio tosha kwa wahafidhina na labda waafrika wote, nazungumzia rais mpya wa Zambia Dr Guy Lindsay Scott ambaye amechukua nafasi baada ya kifo cha rais Michael Satta.
Hili si jaribio dogo hata kidogo, hasa kwa kuzingatia kuwa bado waafrika wengi wanajitofautisha na wazungu kwa vigezo kadha wa kadha lakini uasili, utamaduni na hata rngi zao, na hapa ieleweke kuwa Zambia kiasili ni nchi ya kiafrika ambayo inapaswa kuongozwa na waafrika wenyewe, inashangaza si haba kwa mtu mwenye asili ya Uskochi kuingia Ikulu ya nchi ya Kiafrika akiwakilisha wananchi ambao hafanani nao kinasaba wala kiutamaduni.
Watu wameanza kujipa matumaini hewa kuwa ni rais wa muda, huu pengine ni uvivu wa kufikiri na labda ni kipimo cha kushindwa kutambua uafrika ni nini hasa? Ama rangi au dhana/ideology?
Kwa siasa za Afrika Guy Scott aweza kuwa rais wa kudumu, kujikita kutazama katiba ni kukimbia ukweli namna katiba za nchi zinavyovunjwa barani Afrika ili marais kadha wa kadha waendelee kubaki madarakani, ni muhimu kuzingatia kuwa uzoefu wa siasa za Afrika unaonyesha marais kama Daniel Arap Moi wa Kenya ama Gudluck Jonothan awali walionekana wa mpito lakini hali ikaja kugeuka , wakawa marais waliodumu madarakani, je hili halitatokea kwa Zambia? Tungoje tuone.
Vipi Guy Scott akiwa mwenyekiti wa umoja wa nchi za Afrika (AU), atakapowaongoza marais wenzake wa Afrika kujadili namna ya kupambana na unyonyaji wa mabeberu wa magharibi , tusemeje hapa? Hiki si kipimo kwa vyama vya upinzani barani Afrika kujitafakari namna vinavyojaza wanachama mpaka nafasi za juu za utawala kwa namna Patriotic Front(PF) cha Michael Satta kilivyoiweka Zambia kwenye kizungumkuti?
Kuna mengi ya kungoja hapa, lazima tusubiri tuone namna hali ya mambo itakavyokuwa, dunia inasubiri kuona wahafidhina mithili ya Robert Mugabe watampokea vipi Guy Scott? Watamkubali kama mwafrika mwenzao au watampinga? Wapo wanaoona rais wa kwanza wa Zambia mzee Dr Keneth Kaunda amebarikiwa kuishi muda mrefu kushuhudia nchi yake hiyo aliyoipigania mpaka kupata uhuru mnamo mwaka 1964 ikipitia wakati mgumu kama huu katika kitendawili hiki cha rais Guy Scott!

Nova Kambota ni blogger na mchambuzi wa maswala ya kisiasa anayeishi Dar es salaam nchini Tanzania, anapatikana kwa namba za simu +255(0)712 544237, barua pepe; novakambota@gmail.com, kwa uchambuzi zaidi tembelea blog yake http://www.novakambota.wordpress.com

69 YEARS OF THE UNITED NATIONS (UN)

The assassination of Patrice Lumumba, wars in Darfur and Somalia still the great embarrassment to the International Forum.
index
By Correspondents Nova Kambota and Amani Boniphace,
(+255 712 544237/+255 658503810)
Dar es salaam, Tanzania, Friday 24th Oct 2014,
United Nations General Assembly professed 24 October In 1947, the anniversary of the Charter of the United Nations. UN Day results the anniversary of the access into force in 1945 of the UN Charter with the approval of this founding document by the majority of its signatories, including the five permanent members of the Security Council then United Nations officially came into being in 24 October has been notable as United Nations Day since 1948. In 1971, the United Nations General Assembly suggested that the day be observed by Member States as a public holiday.
Despite a number of successes that has proved by UN still there is a failure which has been witnessed in the days of its lives as it described below;
UNO AND WARS
Since human being has in progress to form societies there have been a struggle for what so termed scarce resources nevertheless of the problem in this world is not scarcity of a resources but it is in how resources are exploited, divided and distributed. This has made the struggle for possessions that enhances into enmity, social struggle and eventually wars for the whole of human race the greatest cause of wars has been for economic reasons.
For the entire life of UNO no even a single instant has been experienced without wars and the way in the direction of it is rocky since there is the wars in one side is economic advantage in another side.
These are roughly wars in the whole world in Africa Hot Spots: Central African Republic (civil war), Democratic Republic of Congo (war against rebel groups), Egypt uprising against Government, Libya war against (Islamist militants), Mali war against (Tuareg and islamist militants), Nigeria war against (Islamist militants), Somalia war against (Islamist militants), Sudan war against (rebel groups), South Sudan (Civil war)
ASIA: 16 Countries and 137 between militias-guerrillas, separatist groups and anarchic groups involved) Hot Spots: Afghanistan (war against Islamist militants), Burma-Myanmar (war against rebel groups), Pakistan (war against Islamist militants), Philippines (war against Islamist militants), Thailand (coup d’etat by army May 2014)
EUROPE: (9 Countries and 71 between militias-guerrillas, separatist groups and anarchic groups involved Hot Spots: Chechnya (war against Islamist militants), Dagestan (war against Islamist militants), Ukraine (Secession of self-proclaimed Donetsk People’s Republic and self-proclaimed Luhansk People’s Republic)
MIDDLE EAST: (8 Countries and 186 between militias-guerrillas, separatist groups and anarchic groups involved) Hot Spots: Iraq (war against Islamic State Islamist militants), Israel (war against islamist militants in Gaza Strip), Syria (civil war), Yemen (war against and between Islamist militants)
AMERICAS: (5 Countries and 25 between drug cartels, militias-guerrillas, separatist groups and anarchic groups involved) Hot Spots: Colombia (war against rebel groups), Mexico (war against narcotraffic groups)
Number of Countries involved in wars is 64, Number of Militias-guerrillas and separatist groups involved is 584.
According to answer.com About 500 people die in a day so about 1,82500 people die in a year.
ASSASSINATIONS
On 17th January 1961 Patrice Lumumba, first and only elected Prime Minister of Congo, was murdered. The environments of his death continued a mystery, the identity of his killers unknown. A 1975 U.S. Senate investigation led by the late Frank Church (D-Idaho) found there was “a reasonable inference” that Eisenhower ratified Lumumba’s assassination, but the committee stopped short of a conclusive finding. According to journalist George Lardner Jr. in the Washington Post, an August of 1960 meeting of Eisenhower with the National Security Council lends to suspicions regarding U.S. contributed. Since the death of Lumumba there is no time that Democratic Republic of Congo has been in Peace.
UNO didn’t learn a lesson from assassination, there is still occurrence of alike assassinations that costs a millions of people lives causalities and destruction of properties and refugees As well as social unrest example Sadam Hussein in Iraq, Muamar Ghadaffi in Libya this is failure of UNO for the whole of her life.
There is a number of specialized agent of UNO which is generally discussed its failures when we are going to enter UN day example those dealing with famine and hunger, Food and Agriculture Organization (FAO), International Fund for Agricultural Development (IFAD) there is more than 900 million people lack of food more that 20000 people die of hungry every day.
International Civil Aviation Organization (ICAO). If we may ask where is Malaysian flight 370 the answer will be is still a remarkable shame in the agency history.
International Labour Organization (ILO) from 1968 to date human generation has accessed education than ever, the hurting truth is the fastly increasing rate of unemployment especially in developing countries.
International Maritime Organization (IMO) reveals that 23,000 Immigrants Have Died Trying To Reach The European Union In The Last 13 Years.
United Nations Educational, Scientific and Cultural Organization (UNESCO). The greatest failure is that there is a deception spread that western culture is the world best culture and the world is mandated to follow it example in when Uganda government passed the laws against mono sexuality USA provoked barriers but this agency didn’t say anything.
International Development Association (IDA), Where’s development?
International Monetary Fund (IMF); there has been multiple debt crises that exist in the world today and developing countries are claiming of conditions that are attached in the debts example in SAP program there were such conditions like reduction of trade barriers, privatization, free trade, free market and made general lives of people around even harder.
Such trend gives the UN not else but a wake up call on immediate need for change, the international forum has been left with very short time to deliver or never at all, sixty nine years is too long period for people to keep on waiting for a biblical manna!

Nova Kambota and Amani Boniphace are the political analysts based in Dar es Salaam, Tanzania. Email; novakmbota@gmail.com and amaniboniphace@gmail.com to read other articles by the same writers you can visit; http://www.novakambota.wordpress.com or http://www.amaniboniphace.blogspot.com

Adolf Hitler ; Kwanini Uingereza na Ufaransa zitabeba dhambi hii milele?

Adolf

Na Nova Kambota,
Jumatano, 26 June 2013

“Unless not later than 11 a.m , British summer time , today September 3rd ,satisfactory assurances have been given by the German government and have reached His Majesty’s Government in London, a state of war will exist between the two countries from that hour”

Hivi ndivyo ujumbe wa serikali ya Uingereza kwenda kwa Adolf Hitler ulivyosomeka siku ya tarehe 3 septemba 1939, masaa machache baadae ulimwengu ukaingia katika kile kilichokuja kujulikana kama vita kuu ya pili ya dunia (1939-1945) ambayo inaelezwa kuwa mpaka leo hii vita hiyo imevunja rekodi ya dunia kwa kuwa vita iliyoteketeza roho za watu wengi zaidi tangu dunia ilipoumbwa.

Tatizo kubwa ambalo wanahistoria wengi wanalifanya ni kujadili janga hili (vita kuu ya pili ya dunia) kwa mtizamo finyu ambao mwisho wake huwa ni kurusha lawama za upande mmoja kwa kumlaumu Adolf Hitler pekee! Kwasababu za kitaaluma, uchambuzi na historia makala hii inajaribu kuibua fikra mpya kwa kutanua mjadala wa nani mwenye kubeba lawama kwa vita hii? Nifate katika makala hii ya kusisimua ambayo itapanua uwezo wako wa kujenga hoja ……………..

Wakati Adolf Hitler anaingia madarakani mwaka 1933 tangu miaka ya mwanzoni ya utawala wake Hitler alionyesha msimamo mkali dhidi ya mkataba wa amani wa Versailles(Versailles Peace Treaty) ambao ulitiwa saini mwaka 1919 kati ya mataifa yaliyoshinda vita kuu ya kwanza ya dunia, kimsingi mkataba huo “uliinyonga” ujerumani kwa kigezo cha kuwa “mwanzilishi” wa vita kuu ya kwanza ya dunia. Hitler alipokuwa kiongozi wa Ujerumani alipingana vikali tena waziwazi na mkataba huu lakini si Uingereza wala Ufaransa waliojitokeza kumpinga Hitler, kwanini?

Ukweli wa mambo ni kuwa licha ya makataba wa amani wa Versailles kutiwa saini lakini kwa nchi nyingi ulitafsirika kuwa si wa amani bali wa kisasi dhidi ya Ujerumani, vyanzo mbalimbali vinathibitisha kuwa hata wakati Hitler alipoanza “ukorofi” wake baada ya kutwaa madaraka nchini Ujerumani wanasiasa wakubwa wa nchini Uingereza akiwemo Neville Chambarlain waliona masharti mengine ndani ya mkataba wa Versailles yalikuwa hayatekelezeki, kwa maana nyingine walibariki uamuzi wa Hitler kukiuka baadhi ya masharti haya.

Sera hii ya kumwacha Hitler kama siyo kumridhisha iliasisiwa na Neville Chamberlain na baadaye kuungwa mkono na Ufaransa ilikuja kujulikana kama “Appeasement Policy” ambayo kimsingi ililenga “kumridhisha” Adolf Hitler na “kuwafariji” Wajerumani kwa kile kilichoonekana kuwa walionewa sana na mkataba wa Versailles. Akiunga mkono sera hiyo ya “kumpoza” Hitler na wajerumani mwenyewe Chambarlain ananukuliwa akisema “If only we could sit down at a table with the Germans and run through all their complaints and claims with a pencil, this would greatly relieve all tension” haya ndiyo yalikuwa mawazo ya waziri mkuu wa Uingereza.

Kuzaliwa kwa sera ya Appeasement siasa za kidezodezo , mwenendo wa kumwacha Hitler kufanya “lolote” ndiko kwa kiwango kikubwa kulikosababisha kuibuka kwa vita kuu ya pili ya dunia 1939. Mataifa yaliyobuni na kutekeleza sera hii ya “kipuuzi” ama “busara” si mengine bali ni Uingereza na Ufaransa. Je kwa kuzingatia hili ni sahihi kumlaumu Hitler pekee? Kwanini Uingereza na Ufaransa zinasafishwa kutoka dhambi hii?

Ni vema ikaeleweka kuwa wanahistoria wote wanakubaliana kuwa Appeasement Policy ilichangia kwa kiasi kikubwa kuibuka kwa vita kuu ya pili ya dunia, tofauti ni kuhusu mantiki ya sera hii, swala la uhalali au uharamu wa sera hii ni lingine isipokuwa la muhimu ni kuwa chimbuko la vita kuu ya pili ya dunia ni sera ya Appeasement ya Uingereza na Ufaransa.

Kwanini Appeasement Policy ni halali?

Miaka ya karibuni kumeibuka kundi la wanahistoria wa kizazi kipya hususani nchini Uingereza ambao wanajaribu kwa kiasi kikubwa kuitetea “Appeasement Policy” kwa nguvu kubwa lengo likiwa ni kulinda heshima ya Neville Chambarlain. Watetezi hawa wanatoa hoja zifuatazo;

(i)Faraja kwa Ujerumani

Mwanzoni viongozi wengi wa dunia wa wakati ule akiwemo Chambarlain wa Uingereza pamoja naye Daladier wa Ufaransa waliamini kuwa kwa kiasi Fulani madai ya Hitler na Wajerumani yana mantiki, ni madai halali kwa kuzingatia ukweli kuwa mkataba wa Versailles uliadhibu vibaya sana Ujerumani, kwa hiyo kila hatua ambayo Hitler alichukua mara moja ilihalalishwa na Uingereza na Ufaransa kwa matumaini kuwa Hitler ataridhika na kutulia.

(ii) Lengo la kuwa na amani ya kudumu

Ni ukweli usiopingika kuwa Uingereza na Ufaransa walihitaji amani ya kudumu barani ulaya, kumbukumbu za mapigano ya vita kuu ya kwanza ya dunia zilikuwa zingali mbichi kwa mataifa haya ya kibeberu, Chambarlain na Daladier kwa pamoja waliamua kumridhisha Hitler kwa kumkubalia yale aliyotaka ilikuwa njia mwafaka ya kumfanya atulie hivyo kuleta amani.

(iii) Hofu ya Ukomunisti

Kwa sababu za kiusalama Uingereza na Ufaransa walihofia kuenea kwa ukomunisti katika nchi za Ulaya ya Mashariki ikiwa watamtumia Joseph Stalin kupenyeza utawala wao katika upande huo wa Ulaya badala yake wakaamua kumtumia Hitler kudhoofisha kuenea kwa ukomunisti katika mataifa ya Poland na Czechoslovakia, kwa kumwacha Hitler(adui mkubwa wa ukomunisti) madarakani kulihakikisha kuwa ukomunisti haupenyi na kusambaa Ulaya ya Mashariki, hii ndiyo sababu Uingereza na Ufaransa hazikutaka kumghasi Adolf Hitler.

(iv)Muda wa kuimarisha majeshi (time to re-arm)

Hoja kubwa inayotumika kuhalalisha Appeasement policy ni kuwa Uingereza haikuwa tayari kwa vita. Mkakati wa kuiandaa Uingereza kwa vita ulianza mwaka 1936 na ulipangwa kumalizika mwaka 1940, ndiyo maana katika mgogoro uliopelekea mkataba wa Munich wa mwaka 1938 Chamberlain alikubaliana na matakwa ya Hitler, kwa kufanya hivyo vita iliahirishwa kwa mwaka mzima kabla ya kulipuka hapo 1939 wakati Uingereza ilikwisha jiandaa vya kutosha( When the crises of 1938 occurred, Britain desperately needed more time to build up its strength. By giving into Hitler’s demands at Munich, war was postponed for a year, and when it did eventually come, Britain had made just enough preparations to survive).

Kwanini Appeasement Policy ni haramu?

Mwezi oktoba 1938, aliyekuwa kiongozi wa chama cha Labour cha Uingereza Clement Attlee alinukuliwa akisema “the events of the last few days are one of the greatest diplomatic defeats this country and France have ever suffered. There can be no doubt that it is a tremendous victory for Herr Hitler. Without firing a shot, he has achieved a dominating position in Europe” hapa ilikuwa baada ya mkataba wa Munich ambapo Chambarlain na Daladier walimruhusu Hitler kuivamia na kuiteka Czechoslavakia nchi iliyokuwa inainukia kiuchumi barani Ulaya.

Ambalo la msingi kuzingatia ni kuwa baada ya mkutano wa Munich si Chambarlain wala Daladier walioamini kuwa wamefanya jambo sahihi kumruhusu Hitler kuivamia Czechoslovakia, wote hawakuliamini hili hata kama kwa kuwapotosha waingereza Chambarlain ananukuliwa akisisitiza kwa kusema “I believe it is peace for our time” naye Daladier alipofika uwanja wa ndege wa Paris kinyume na matarajio yake wafaransa walimpokea kwa shangwe kwasababu walishaleweshwa na propaganda naye kwa kutambua ukweli huo aliishia kuwaita wajinga “at the airport Daladier turned up his coat collar to protect his face from the rotten eggs he expected from the crowd. To his astonishment there were no eggs or shouts of ‘We are betrayed’. Instead they were actually cheering him-shouting ‘Vive Daladier ‘ , ‘ Vive la Paix ‘ , Vive la France!’ Daladier turned to a collegue and whispered, ‘The fools!’ . Hapa jambo la kuzingatia ni kuwa hata viongozi wa Uingereza na Ufaransa wenyewe waliona wamekosea, wamekosea kwa sera yao ya Appeasement, sera hii ilikuwa haramu kwa kuzingatia hoja hizi;

(i)Uingereza na Ufaransa hawakumwelewa Hitler kiundani(The appeasers misjudged Hitler)

Chambarlain na Daladier walifanya kosa kubwa sana la kumchukulia Hitler kama mwanasiasa makini mwenye uwezo wa kutambua mema na mabaya na ambaye alikuwa tayari kujadiliana. Hawakumwelewa Hitler mpaka walipojikuta wamekwishachelewa sana, baadae sana walikuja kutambua kuwa walikuwa wanacheza na dikteta hatari ambaye kila walipojishusha na kumkubalia matakwa yake yeye alitafsiri kuwa ni udhaifu, kadri walivyompa ndivyo alivyohitaji zaidi(The more they gave him , the more he demanded).

(ii)Appeasement ilikuwa na udhaifu wa kimantiki

Uingereza na Ufaransa walihofia sana vita nyingine kiasi cha kuiruhusu Ujerumani kuvunja makubaliano ya kimataifa pasipo adhabu yoyote, mwishowe waliacha Hitler kuivamia Czechoslovakia kwa ahadi hewa zisizo na maana yoyote. Sera ya Appeasement haina maneno mengine ya kuielezea isipokuwa udhaifu na uoga(Appeasement was simply another word for weakness and cowardice).

(iii) Uingereza na Ufaransa zilishindwa kutumia vizuri fursa za kumzuia Hitler

Uingereza na Ufaransa kwa pamoja walipoteza muda mwingi kuridhia matakwa ya Hitler kiasi cha kushindwa kutumia fursa nyingi za kumzuia zilizojitokeza. Mfano Adolf Hitler mwenyewe ana kiri kuwa ikiwa Ufaransa na Uingereza wangezuia mpango wake wa kuimarisha jeshi lake katika eneo la Rhineland mwaka 1936, basi asingekuwa na mbadala zaidi ya kuachana na mpango huo lakini kwa bahati mbaya Uingereza na Ufaransa walifumba macho na kumwacha Hitler aendelee na vurugu zake kwa maana nyingine walitumia sera dhaifu ya Appeasement. Uingereza na Ufaransa walitumia muda mwingi kungoja kusikiliza Hitler atadai nini ili wampe badala ya kuandaa mikakati ya kumzuia kuvunja makubaliano ya kimataifa.

Uingereza na Ufaransa wana dhambi ya kubeba!

Ikiwa Uingereza na Ufaransa walibuni na kutekeleza Appeasement Policy kwa lengo la kuzuia vita isitokee huku wakijua wazi kuwa Hitler hakuwa mtu wa kutosheka hata kidogo, je kwanini mataifa haya yasibebe lawama? Mara baada ya kuzuka kwa vita kuu ya pili ya dunia 1939 Chambarlain anakaririwa akisisitiza “This is a sad day for all of us, and to none is sadder than to me. Everything that I have worked for, everything that I have belived in during my public life, has crashed into ruins” hii ndiyo kauli ya Neville Chambarlain kiongozi wa Uingereza aliyechangia kwa kiasi kikubwa kuitumbukiza dunia katika vita kuu ya pili ya dunia sambamba na Ufaransa .

Ni ngumu kueleza chimbuko la vita kuu ya pili ya dunia pasipo kuihusisha Uingereza na Ufaransa, si sahihi kuchambua uovu wa Adolf Hitler bila kumhusisha Chambarlain na Daladier! Kwa kutambua kabisa Uingereza na Ufaransa “walilea” tatizo ambalo liliitumbukiza dunia kwenye janga la vita, Adolf Hitler ni mwovu kweli ,ni mhanga wa kihistoria , ni zao la sera dhaifu za Uingereza na Ufaransa ambazo pasi na shaka hazina budi kugawana zigo la lawama na Ujerumani kwa kusababisha vita kuu ya pili ya dunia 1939-1945, pasipo ubishi wowote Uingereza na Ufaransa kwa pamoja zinapaswa kuibeba dhambi hii ya kihistoria.

Mchambuzi&Mwanaharakati